Nairobi. Wananchi wa Kenya wameendelea kuaga mwili wa aliyekuwa Rais wa Kenya, Daniel Arap Moi baada ya kuwasili kwa siku ya pili katika majengo ya Bunge kutoka hifadhi ya maiti ya Lee jijini Nairobi.
Mwili huo umewasili leo asubuhi ukiwa katika mavazi tofauti na yale ya jana; jana ulivalishwa suti ya rangi la bluu na viatu vya kahawia, na leo uko katika suti ya kahawia na viatu vyeusi.
Tofauti na ilivyoeleka kwa Watanzania kwa kuweka mwili ndani ya jeneza, mwili wa Moi umelazwa juu ya meza ukiwa umewekewa mto.
Wananchi wa Kenya wameanza kufika kuanzia alfajiri saa 11 na mwili ulipowasilia walianza kupita kwa foleni ndefu kutoa heshima zao za mwisho.
Rais mstaafu, Mwai Kibaki amekuwa miongoni mwa viongozi waliofika siku ya pili Jumapili kumuaga mtangulizi wake Moi ambaye mauti yalimkuta katika Hospitali ya Nairobi alikokuwa anapata matibabu.
Kibaki aliyeambatana na Naibu Rais, William Ruto alifika katika majengo ya Bunge saa 5:00 asubuhi.
Pia Soma
- Moto wawaka maaskofu KKKT
- Mafuriko yafunga barabara ya Songwe Tanzania
- Raia wa Poland adakwa akituhumiwa kulima bangi Tanzania
Mkuu wa utumishi wa umma, Joseph Kinyua alisema shughuli ya kushuhudia mwili wa Moi iliyoanza Jumamosi itamalizika Jumatatu
Jumanne, shughuli ya kumwaga kiongozi huyo kitaifa itafanyika katika Uwanja wa Nyayo jijini Nairobi.
Baada ya hapo mwili huo utasafirishwa kwenda nyumbani kwake Kabarak, Nakuru kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika Jumatano Februari 12.