Mwandishi wa Uganda anayetuhumiwa kutuma taarifa za kashfa kuhusu rais na mtoto wake wa kiume kwenye mtandao wa Twitter amefunguliwa mashtaka mahakamani, wiki kadhaa baada ya kukamatwa.
Kakwenza Rukirabashaija alishtakiwa kwa makosa mawili ya mawasiliano ya kukera na amepelekwa gerezani hadi Januari 21, atakapofikishwa tena mahakamani.
Wakili wake Eron Kiiza alisema mwandishi huyo alikuwa akichechemea, na aliiambia mahakama kuwa afya yake inadhoofika. Wakili huyo hapo awali alisema kuwa mteja wake aliteswa aliipokuwa kizuizini.
Bw Rukirabashaija alikamatwa mwezi Disemba na wiki iliyopita, mahakama iliamuru aachiliwe bila masharti lakini mamlaka haikuzingatia agizo hilo.