Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mwaka mmoja tangu kifo cha Walibora, twamkumbuka vipi marehemu!

9f557c9269551fe7 Mwaka mmoja tangu kifo cha Walibora, twamkumbuka vipi marehemu!

Tue, 13 Apr 2021 Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke

Kauli ya Mhariri: Makala haya ni kutoka kwa Amin Kweyu Watako ambaye ni mwalimu wa Kiswahili na mdadavuaji wa masuala ya lugha. Kumbuka kauli iliyotolewa hapa ni ya mwandishi binafsi wa makala haya na wala sio msimamo wa TUKO.co.ke.

Wasanii wengi wamekizungumzia mno kifo. Vitabu vya dini vimeyasema mengi kukihusu kifo. Hata na wahenga wakasema kuwa kuugua ni sunna, kufariki dunia ni faradhi. Kwa kifupi, kila nafsi itayaonja mauti.

Pia Soma: Jameni serikali fungueni pingu za mashabiki wanataka kuingia viwanjani

Pia Soma: Hizi Bei za Mafuta Zinatukandamiza, Wakenya Tunaumia Sana Serikali!

Ndio maana katika dini zetu tunayazuru makaburi na kuwatilia dua ndugu na jamaa zetu waliotangulia mbele za haki. Lakini tukishatoka makaburini, sisi hujiuliza ni lini pia na sisi tutalazwa makaburini na watu watasema nini kutuhusu, au ni nini (amana) tutakwenda nayo makaburini. Na ni kwa vipi tutakabiliana na adhabu za kaburini.

Leo hii tunavyozungumza ndugu yangu ni kuwa ulimwengu wa Kiswahili duniani unaadhimisha mwaka mmoja tangu mwandishi na mwanahabari Profesa Ken Walibora Waliaula kutangulia mbele za haki. Marehemu Ken aliandika na kuandika. Hadi vitabu vikatii. Alitangaza na kutangaza. Hadi matangazo yakamkubali. Nakumbuka alipenda kujiita ‘mtoto wa mwalimu’. Na kweli alifuata nyayo za wazazi. Alifunza kweli!

Pia Soma: Kapedo: Eneo hili limekuwa pango na aburi kubwa la mauti



Vipi kuyahusu mazingira alimofia ndugu yetu? Na hapo ndipo ulipo mzizi wa fitina. Hadi leo hii uchunguzi ungali kuendelea kukihusu kifo cha Ken. Halijasemwa jambo. Kimya ji! Hadi lini? Aligongwa na gari ndugu yetu ati! Eneo hilo, hasa barabara hiyo ingekuwa imepewa heshima ya Walibora. Tungekuwa na WALIBORA ROAD. Lakini wepi. Majina ya barabara, viwanja na majengo wanapewa wanasiasa tu. Ama kweli dunia tambara bovu!

Aliaga dunia ndugu yetu kukiwa na hizi funga funga za nchi na kafyu! Mwaka mmoja baadaye, makufuli ya funga funga za nchi yangalipo. Baadhi ya jamaa walijaaliwa kufika nyumbani kwao marehemu huko Trans-Nzoia na kuifariji familia. Mola Awabariki nyote. Tulikuwa tukipanga na ndugu yangu mshairi Hassan bin Chui kwa ushirikiano na kaunti ya Trans-Nzoia, ili mashabiki wafurike mjini Kitale wakati huu wa maadhimisho ya mwaka mmoja tangu kifo kutupoka ndugu yetu. Lakini wepi. Kazi ya Mola haina makosa. Aliimba Marjan Rajab.

Pia Soma: Wachezaji vichaa! Nidhamu uwanjani ni sehemu ya mchezo, bila hiyo lazima nuksi itatawala

Jumamosi hii mashabiki wa marehemu Ken watapata nafasi ya kumkumbuka kupitia kikao maalum cha Zoom ambacho kimeandaliwa na wadau mbali mbali akiwemo dada yetu mshairi Phibian Muthama.

Ndugu Ken, lala salama. Corona ulioiacha ingali kututafuna! Ni mwaka mmoja sasa. Wasalimu wenzio huko. Kina Abu Marjan, Mustafa Iddi, Ahmed Dharwesh, Abdallah Mwasimba, Waweru Mburu, Billy Omalla… Orodha ni ndefu.

HITIMISHO: Kufariji ni kumpa pole mtu ambaye amefikwa na simanzi ya kuondokewa na jamaa yake.

Makala haya yameandikwa na Amin Kweyu, unaweza kuwasiliana naye kupitia [email protected].

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.

Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke