RAIS Uhuru Kenyatta ametangaza kurefusha kwa siku nyingine 60 vizuizi vya kukabiliana na janga la virusi vya corona.
Aidha, amesema shule bado zitaendelea kufungwa hadi usalama wa wanafunzi utakapozingatiwa. hadi kufikia mwaka 2022.
Akizungumza wiki iliyopita kwenye kongamano la wadau wa mapambano dhidi ya virusi vya corona, Rais Kenyatta alisema masharti ya kutotoka majumbani sasa yataanza kutekelezwa saa 5:00 usiku hadi saa 10:00 alfajiri, ambapo awali yalikuwa yakitekelezwa kuanzia saa 3:00 usiku.
Hata hivyo, baa na vilabu vimeruhusiwa kufunguliwa baada ya kufungwa kwa miezi sita lakini wakitakiwa kuzingatia kikamilifu masharti yaliyotangazwa na wizara ya afya ya kujilinda dhidi ya maambukizi ya corona.
Kuhusu suala la tarehe ya kufunguliwa kwa shule, Rais Kenyatta hakutaja tarehe mahususi, akisema ni bora usalama wa wanafunzi ukazingatiwa kabla ya kufunguliwa kwa shule.
Mpaka sasa Kenya imerekodi visa zaidi ya 39,000 vya maambukizi ya virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa wa covid-19, huku watu 700 wakifariki dunia kutokana na ugonjwa huo.
Waziri wa Elimu, Profesa George Magoha, atatangaza tarehe ya kufunguliwa shule pindi usalama katika shule zote utakapozingatiwa. Jumatatu iliyopita walimu wa shule walianza kufanya maandalizi ya kufunguliwa kwa shule zao.
Aidha, idadi ya waumini makanisani na wanaoruhusiwa kushiriki kwenye shughuli za mazishi pia imeongezwa kutoka 100 hadi 200.
Kwa kipindi cha miezi sita tangu masharti hayo yaanze kutekelezwa, matukio ya uhalifu yamepungua kwa asilimia 21, huku misongamano ya magari ikipungua kwa wastani wa asilimia 10.