Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Muammar Gaddafi: Baada ya Miaka 10 Walibya wana majuto?

Mammar Gaddafi Aliyekua Rais wa Libya,Muammar Gaddafi

Thu, 5 Aug 2021 Chanzo: BBC

Miaka kumi tangu kuuawa kwa kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi, mwanawe wa kiume Saif al-Islam alijitokeza wiki iliopita na kusema anataka kurejea nyumbani na kuwania Urais wa Taifa lake.

Hatua hiyo ya Islam imezua mjadala nchini mwake ya iwapo kuna majuto miongoni mwa Walibya kuhusu yaliyomsibu kiongozi wao wa miaka Zaidi ya 40 .

Hadi sasa bado haijulikani athari za hatua ya Islam kutaka kurejea Libya na kurejea Madarakani miaka 10 baada ya baba yake na baadhi ya kaka zake kuuawa katika mapinduzi ya Umma.

Lakini ili kufahamu hisia katika nyoyo za Walibya wengi kuhusu hali ilivyo nchini humo,ni vyema kujua kwa ufupi historia ,makosa na mafanikio ya Gaddafi .

Katika miaka yake ya kwanza baada ya kuchukua madaraka kupitia mapinduzi yasiyo na umwagikaji wa damu mnamo mwaka wa 1969 ,Gaddfai alikuwa kila walichohitaji Walibya .

Aliahidi kuwatumia watu maskini na hata alichukia sana uharibifu wa raslimali za umma .Mwenyewe kwa siku kadhaa alijiendesha katika gari lake akisema Mawaziri hawakuhitaji madereva na walinzi .Hilo lilibadilika alipojikita ongozini na baadaye ulinzi na magari ambayo Gadafi alimiliki na kutumia katika misafara yake iliwaacha wengi vinywa wazi .

Kama mfuasi mkubwa wa Rais Gamal Abdel Nasser wa Misri (hata alichukua cheo hicho hicho cha kijeshi, alijipandisha cheo kutoka kwa kapteni hadi kanali baada ya mapinduzi), Gaddafi kwanza alianza kushughulikia urithi usiofaa wa kiuchumi wa utawala wa kigeni.

Kwa Nasser, ilikuwa Mfereji wa Suez. Kwa Gaddafi, yalikuwa mafuta.

Akiba kubwa ya mafuta ilikuwa imegunduliwa nchini Libya mwishoni mwa miaka ya 1950, lakini uchimbaji huo ulidhibitiwa na kampuni za kigeni za mafuta, ambazo zilipanga bei kwa faida ya watumiaji wao wa nyumbani na kufaidika na nusu ya mapato.

Gaddafi alitaka kujadiliwa tena kwa mikataba hiyo, na kutishia kufunga uzalishaji ikiwa kampuni za mafuta zitakataa.

Ufadhili wa makundi ya waasi na mauji ya wakosoaji wake.

Bila kudhibitiwa na vizuizi vyovyote vya kawaida vya utawala, Gaddafi aliweza kupeleka kampeni yake ya kupinga ubeberu kote ulimwenguni, kufadhili na kusaidia vikundi vya wapiganaji na harakati za wapinzani popote alipowapata.

Alilenga pia wahamiaji wa Libya, kadhaa ambao waliuawa na vikosi vya mtandao wa majasusi wa Libya.

Ikiwa serikali zingekuwa tayari kupuuza ukiukaji wa haki za binadamu wa Gaddafi nchini Libya, na kuteswa kwa wapinzani nje ya nchi, lilikuwa jambo tofauti wakati ilimjia akiunga mkono vikundi vilivyotumia ugaidi katima ngome zao .

Bomu katika klabu cha usiku kilichotumiwa na wanajeshi wa Marekani huko Berlin mnamo 1986, kulaumiwa kwa maajenti wa Libya, ni tukio ambalo lilimuweka katika mkondo wa kujipata mashakani baadaye .

Rais wa Marekani Ronald Reagan aliamuru shambulio la angani dhidi ya Tripoli na Benghazi kulipiza kisasi kwa wanajeshi hao wawili na raia mmoja waliouawa na makumi ya waliojeruhiwa, ingawa hakukuwa na uthibitisho dhahiri zaidi ya "mazungumzo" ya kijasusi kwamba Libya ilikuwa imeamuru shambulio hilo.

Kisasi cha Marekani kilikusudiwa kumuua "mbwa mwendawazimu wa Mashariki ya Kati", kama Bwana Reagan alivyokuwa akimuita Gaddafi lakini ingawa kulikuwa na uharibifu mkubwa na idadi isiyojulikana ya vifo vya Walibya - pamoja na, ilidaiwa, binti wa Gaddafi - kanali mwenyewe aliibuka bila kujeruhiwa.

Shambulio la bomu dhidi ya ndege ya Pan-Am 103 juu ya mji wa Uskochi wa Lockerbie mnamo 1988 ilikuwa hatua nyingine kubwa iliyofuata, na kusababisha vifo vya watu 270 angani na ardhini, kitendo kibaya zaidi cha ugaidi kuwahi kushuhudiwa nchini Uingereza.

Hatua ya awali ya Gaddafi kukataa kuwakabidhi washukiwa wawili wa Libya kwa mamlaka ya Uskochi kulisababisha kipindi cha mazungumzo cha muda mrefu na vikwazo vya UN, mwishowe kumalizika mnamo 1999 na kujisalimisha kwao na kuanza kwa kesi .

Ilikuaje hadi kifo cha 'mkombozi' wa watu?

Wakati wimbi la mapinduzi lilipoanza kuvuma kupitia ulimwengu wa Kiarabu kutoka Tunisia mnamo Desemba 2010, Libya haikuwa juu ya orodha ya watu wengi wa "nani ajaye".

Gaddafi kufikia wakati huo alikuwa ameshatambulika kama mtawala wa kimabavu ambaye alivumiliwa kwa miaka na raia. Lakini hakutambuliwa sana kama kibaraka wa magharibi kama viongozi wengine wa Kiarabu, walioshutumiwa kwa kuweka masilahi ya nje mbele ya maslahi ya watu wao wenyewe.

Aligawanya mali ya nchi kwa usawa - ingawa utajiri wa familia yake mwenyewe kutoka mapato ya mafuta na mikataba mingine ilikuwa ngumu kupuuza na ugawaji ulifanywa zaidi lengo la kununua uaminifu kuliko kukuza usawa.

Uhusiano wake na nchi za nje ulikuwa umevurugika na vikwazo vikaanza kuwabana Walibya katika nyanja zote hasa baada ya kuzuiwa kuuza mafuta yao mwaka wa 1982 . Kisha umoja wa Mataifa pia ukazidisha vikwazo kufuatia shutuma kwamba Libya ilikuwa ikiunga mkono mashambulizi na vitendo vya kigaidi .

Utawala wake ulianza kuchukua sura ya udikteta wakati wananchi walipoanza kunung'unika na kampeni za kuwakandamiza wapinzani zikafuata . Hali iliongezwa kasi maandamano dhidi ya utawala wake yalipoanza mwaka wa 2011.

Maandamano hayo yaligeuka na kuwa vita vya wenyewe kwa wenyewe huku Gaddafi akiapa kamwe hangetoroka nchi yake hadi shambulizi la NATO lilipolenga msafara wake na kisha akashikwa na kundi la wapiganaji waliokuwa wakipambana na wanajeshi wake .

Kufikia wakati huo wengi wa waliokuwa wakimuunga mkono walikuwa wameshamuacha na kujiunga na makundi ya upinzani yaliyojihami na kuendeleeza harakati za kumtimua madarakani . Mojawapo ya makundi hayo ndio yanayolaumiwa kwa kumuua siku hiyo ambayo shambulizi la angani la NATO lililenga msafara wake alipokuwa akitoroka mapigano .Ulikuwa ni mwisho mbaya kwa Gaddafi ambaye alikuwa ameiongoza nchi yake kwa miaka 42.

Chanzo: BBC