Msichana mwenye umri wa miaka tisa alianguka na kufa nchini Zimbabwe wakati alipokuwa akiwakimbia wachezaji wa ngoma ya asili waliokuwa wakiicheza ngoma hiyo katika kitongoji cha Mabvuku, kilichopo katika mji mkuu, Harare.
Taarifa ya polisi iliyotolewa Jumatano imesema kuwa msichana huyo alifariki baada ya kuanguka chini alipokuwa akiwatoroka wachezaji wa ngoma ya Nyau katika shule iliyopo Mabvuku siku ya Jumatatu.
Uchunguzi unaendelea kuhusu tukio hilo, ilisema polisi bila kutoa taarifa zaidi.
Wachezaji wa ngoma ya Nyau, ambao pia hujulikana kama zvigure/izitandari katika kabila la Shona, mara nyingi huwatisha watoto kwa uchezaji na mavazi yao ya kutisha.
Licha ya uchezaji wake wa kuvutia, wanangoma huhusishwa na imani nyingi miongoni mwa watu wazima, lakini watoto wadogo, huwaona kama majitu ya kutisha, vinasema vyombo vya habari nchini humo.
Wachezaji wa ngoma ya Nyau wanatoka katika jamii ya Chewa inayopatikana kaskazini - magharibi mwa Zimbabwe. Jamii ya kabila hilo pia wanapatikana katika mataifa ya Malawi na Zambia.
Wachezaji wa ngoma hiyo husaidia kurithisha utamaduni na historia kwa watu wa jamii ya Chewa.