Watu wenye silaha wameshambulia msafara wa timu ya Rais wa Nigeria, Muhammadu Buhari huko Katsina, jimbo anakotoka kaskazini mwa nchi hiyo.
Watu wawili walipata majeraha katika msafara wa awali wa walinzi, maafisa wa itifaki na vyombo vya habari, kulingana na taarifa ya msemaji wa rais Garba Shehu.
Msafara huo ulikuwa umeenda kabla ya safari ya rais kuelekea mji wake wa Daura kusherehekea sikukuu ya Eid-ul-Adha ya Waislamu wikendi hii wakati washambuliaji walipowafyatulia risasi.
Hata hivyo jeshi lilifanya mashambulizi ya kujibu na kuwazuia na shambulizi lao, ofisi ya rais ilisema.
Katsina ni mojawapo ya majimbo ya kaskazini-magharibi mwa Nigeria yaliyoathiriwa na vitendo vya uhalifu wa majambazi. Watu wengi wameuawa na maelfu kutekwa nyara katika eneo hilo tangu 2015.