Afisa wa jeshi la wanamaji aliyetajwa na serikali ya Gambia kuwa mpangaji mkuu wa njama ya mapinduzi yaliyotibuliwa mwezi Disemba mwaka jana amepatikana na hatia ya uhaini na kuhukumiwa kifungo cha miaka 12 jela.
Mahakama kuu siku ya Jumanne iliamua kwamba Lance Koplo Sanna Fadera alipanga na kujaribu kupindua serikali iliyochaguliwa kidemokrasia ya Rais Adama Barrow.
Mamlaka ilikuwa imemshtaki Fadera na wanajeshi wengine saba kwa uhaini, kula njama na kuchochea uasi kwa madai ya kuhusika katika jaribio la mapinduzi ya 2022.
Mahakama iliwaachilia huru maafisa wengine watatu wa kijeshi siku ya Jumanne.
Mwanajeshi mwingine amekuwa akikimbia tangu jaribio la mapinduzi lililoshindwa na anachukuliwa kuwa mtoro.
Mahakama pia ilimuachia huru afisa wa polisi na raia wawili waliokuwa wameshtakiwa kwa kuficha uhaini na kula njama ya kutenda uhalifu.
Kabla ya Rais Barrow kuingia madarakani, nchi hiyo ya Afrika Magharibi ilitawaliwa kwa miongo miwili na Yahya Jammeh, ambaye alichukua mamlaka katika mapinduzi ya mwaka 1994, na kuzuia majaribio kadhaa ya kutaka kumpindua, kabla ya kushindwa katika uchaguzi wa 2016.