Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mpaka wa Benin na Niger bado umefungwa!

Mpoaka Niger Benin.png Mpaka wa Benin na Niger bado umefungwa!

Tue, 27 Feb 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Siku mbili baada ya tangazo la kuondolewa kwa vikwazo vizito zaidi vya kikanda dhidi ya Niger, mpaka wake na Benin na kituo chake kikuu cha kuelekea baharini, umesalia kufungwa siku ya Jumatatu, wakaazi wa Gaya, mji ulio karibu na Benin, wameliambia shirika la habari la AFP.

"Kwa upande wa Niger, bado hakuna mabadiliko: hadi sasa mpaka bado haujafunguliwa kwa hivyo bado tunasubiri," Fhadel Alou, mwandishi wa habari wa kituo cha redio cha kibinafsi huko Gaya, ameliambia shirika la habari la AFP. "Mpaka umefunguliwa tena upande wa Benin," kulingana na mwandisi huyo wa habari. "Mpaka wetu na Benin bado umefungwa," wamethibitisha viongozi wawili wa eneo hilo waliochaguliwa.

"Benin iliondoa vizuizi vyake jana (Jumapili), lakini imefungwa upande wa Niger," wamesema wakazi wanaoishi upande wa Benin.

Kulingana na vyanzo hivi, "kifaa kilichowekwa (tangu kufungwa) na jeshi la Niger kwenye daraja la kuzuia njia bado kipo". Daraja hili linaweka mpaka wa nchi hizo mbili zinazotenganishwa na Mto Niger.

Katika kukabiliana na mapinduzi ya kijeshi yaliyotokea Julai 26 nchini Niger, Benin ilitekeleza vikwazo vilivyoamuliwa Julai 30 na Jumuiya ya Kiuchumi ya Afrika Magharibi (ECOWAS), ikiwa ni pamoja na kufungwa kwa mpaka wake na jirani yake Niger. Niger pia ilikuwa imefunga mpaka wake na Benin.

Vikwazo vizito zaidi kati ya hivi, ikiwa ni pamoja na kufungwa kwa mipaka, viliondolewa siku ya Jumamosi. Kabla ya kufungwa huku, ukanda wa Benin ulipokea 80% ya mizigo ya Niger kupitia bandari ya Cotonou, kilomita elfu moja kutoka Niamey. Vikwazo vya ECOWAS dhidi ya Niger pia vimesababisha kushuka kwa mapato ya bandari nchini Benin.

Mwishoni mwa mwezi wa Desemba, Benin ilitangaza kuwa iliondoa hatua ya kusimamishwa kwa uagizaji wa bidhaa zinazopitia Niger kupitia bandari ya Cotonou. Bomba kubwa la mafuta linalounganisha kusini-mashariki mwa Niger na pwani ya Benin, lililoagizwa mwanzoni mwa mwezi wa Novemba mwaka jana ili kuruhusu uuzaji wa mafuta ghafi ya Niger katika soko la kimataifa kuanzia mwezi wa Januari, pia ni suala linalotia wasiwasi kwa nchi hizo mbili.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live