Zaidi ya ekari 40,000 za misitu zimeharibiwa na moto wa nyikani katika milima ya Aberdare katikati mwa Kenya.
Moto huo, ambao uliripotiwa kwa mara ya kwanza katika misitu ya Hifadhi ya Kitaifa ya Aberdare wiki mbili zilizopita, umeendelea licha ya mamia ya wazima moto kutumwa katika eneo hilo kujaribu kuuzuia.
Askari wawili wa Shirika la Huduma ya Wanyamapori (KWS) waliuawa gari lao lilipobingirika walipokuwa wakikimbilia eneo la tukio siku ya pili.
Bakari Mungumi, kutoka kwa Hifadhi ya Milima ya KWS, aliambia BBC uchunguzi kuhusu chanzo cha moto huo bado unaendelea.
Ukame wa muda mrefu husababisha misitu kukauka, hali ambayo inaweza kuwa hatari moto ukizuka.
Huu sio moto wa kwanza kutokea katika eneo hilo.
Mnamo mwaka 2012, moto uliharibu zaidi ya ekari 70,000 za msitu.