Rais wa zamani wa Kenya Uhuru Kenyatta amesema nyumba ya mwanaye wa kiume imevamiwa.
Akizungumza na waandishi wa habari Bw Kenyatta amesema: ‘’nimepigiwa simu na mtoto wangu wa kiume akaniambia kuwa wakati alipokuwa akitaka kutoka nyumbani kwake aliambiwa kuna watu wanaodai kuwa ni maafisa wa upelelezi DCI, waliokuwa ndani ya gari lenye nambari za usajili za Sudan wanaotaka kuzungumza naye’’
Bw Uhuru amesema alimwambia mwanaye asitoke nyumbani kwake na badala yake aliamua kwenda kwa mwanaye kuwaona watu hao.’’ Nilitaka niende niwaulize ni nini wanatafuta kwa mwanangu’’, alisema.
Hata hivyo anasema alipofika alikuta tayari watu hao wameondoka.
Bw Kenyatta amesema ‘'Mnapaswa kunijia mimi, muache kuitisha familia yangu!’’…Msifikirie mnaweza kunitishia, mnaweza kutokubaliana nami …lakini sitaruhusu familia yangu kushambuliwa’’, alisema.
Wiki hii mama yake Uhuru Kenyatta, Mke wa Rais wa Kwanza wa Kenya, Mama Ngina Kenyatta aliondolewa walinzi wake suala lililoibua hisia miongoni mwa Wakenya.
Akizungumzia suala hilo Bw Kenyatta alisema ‘’Usidhani unaweza kumtishia mwanamke mkongwe na wajukuu zake ili kunitisha mimi…Unafahamu nilipo saa 24, njoo nijie mimi’’
Rais William Ruto amekuwa akimshutumu Uhuru Kenyatta kufadhili maandamano ya upinzani nchini yanayoongozwa na kinara wa upinzani Raila Odinga.