Cairo, Misri. Raia wa Ujerumani amefariki dunia nchini Misri kutokana na virusi vya corona (covid-19).
Mjerumani huyo ameweka rekodi ya kuwa mtu wa kwanza kufariki dunia kutokana na virusi hivyo barani.
Wizara ya afya ya Misri ilisema kuwa mgonjwa huyo alipoteza maisha jana ikiwa ni siku tatu baada ya kugundulika kuwa na maambukizi ya virusi hivyo.
Wizara hiyo ilisema raia huyo wa Ujerumani mwenye umri wa miaka 60 alionesha dalili za homa na kufikishwa katika Hospitali ya Hurghada Machi 6.
Wizara hiyo ilisema kuwa baada ya vipimo ilithibitika kwamba raia huyo ambaye alifika nchini humo kwa shughuli za kitalii alikuwa na virusi vya corona.
Hata hivyo, inaelezwa kwamba awali mgonjwa huyo alikataa kupelekwa katika wodi maaalum iliyowekwa kwa ajili ya kuwahudumia watu walioambukizwa na ugonjwa huo.