Jaguar alifanyiwa upasuaji kwenye goti siku ya Jumatatu, Juni 28Mbunge huyo alipata jeraha kwenye goti lake mwaka wa 2019 na amekuwa akihisi uchungu tangu wakati huoHali yake ilidoroa hivi maajuzi baada ya kurejea nchini kutoka India na madaktari wakamshauri afanyiwe upasuajiMbunge wa Starehe Charles Njagua alifanyiwa upasuaji siku ya Jumatatu, Juni 28, 2021 kwenye goti lake katika hospitali ya MP Shah jijini Nairobi.
Kupitia kwenye mitandao ya kijamii, msanii DK Kwenye Beat alipakia video iliyomuonyesha Jaguar akiondolewa kwenye chumba cha upasuaji.
"Jaguar alifanyiwa upasuaji hii leo Jumatatu, Juni 28 majira ya saa kumi na moja alfajiri katika hospitali ya MP Shah, goti lake lilikuwa likimsumbua tangu mwaka wa 2019 na amekuwa akihisi uchungu sana, " DK Kwenye Beat aliambia Citizen Digital.
Jaguar anasemekana kuzidiwa na uchungu wiki mbili zilizopita baada ya kurejea nchini kutoka India, madaktari walimshauri afanyiwe upasuaji wa goti.
Taarifa za kuaminika ziliarifu kwamba Jaguar aliumia goti lake kwenye vurugu iliyotokea kati ya wafanyabiashara wa masoko ya Muthurwa, Marikiti na Wakulima mwaka wa 2019.
" Nilipokuwa nikiwahutubia wafanyabiashara, maafisa wa polisi walirusha vitoa machozi na hapo ndipo nilijeruhiwa katika harakati ya kujaribu kuyanusuru maisha yangu," Alisema Jaguar awali.
" Sikujua nimevunjika mguu wakati huo, baadaye niliona goti langu likianza kufura," Aliongezea Jaguar."
Jaguar kupitia video aliyoipakia mitandaoni alisema amechoshwa sana na kuwa mgonjwa na alimuomba Mungu amuponye.
Mashabiki mitandaoni walimtakia afueni ya haraka pindi alipopakia video yake akiwa katika hali mbaya.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.
Tazama Video Kemkem za Kusisimua Kutoka hapa TUKO.co.ke.