Sierra Leone imetangaza hali ya dharura ya janga la taifa baada ya kuongezeka kwa visa vya matumizi ya madawa ya kulevya. Amri ya Rais Julius Maada Bio inafuatia kuongezeka kwa matumizi ya dawa ya kutengeneza inayojulikana kama Kush. Dawa hiyo ya mihadarati inayolevya sana ni mchanganyiko wa bangi, tentanyl na tramadol, ambayo ni dawa kali ya maumivu. Imeelezwa kuwa Kush imesababisha mamia ya vifo na kuwafanya watumiaji wengi kuwa wagonjwa kiakili.
Dawa hiyo ya mihadarati ilionekana kwa mara ya kwanza katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi miaka minne iliyopita. Kush inatumika sana pia katika nchi jirani ya Liberia. Rais Julius Maada Bio
Rais Bio amesema kupitia amri aliyotoa kwamba, kikosi kazi kitaundwa kutekeleza mkakati wa pande nyingi wa kukabiliana na matumizi ya madawa ya kulevya.
Wafanyakazi wa kada ya matibabu nchini Sierra Leone wamekaribisha agizo hilo lililotolewa na rais Bio.
Ikiwa ni nchi iliyokumbwa na vita vya muda mrefu vya wenyewe kwa wenyewe vilivyomalizika mwaka 2002, na mlrpuko mbaya wa Ebola miaka minane iliyopita, Sierra Leone, ambayo ina utajiri mkubwa wa madini ya almasi imejitahidi kukuza uchumi wake na ukosefu wa ajira kwa vijana ambao ungali ni wa kiwango cha juu.../