SERIKALI nchini Afrika Kusini imepiga marufuku unywaji wa pombe hadharani wakati wa Sikukuu za Pasaka na kuwataka wananchi kuendelea kuzingatia kanuni za kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona.
Akitoa agizo hilo juzi, Waziri wa Utawala na Masuala ya Utamaduni, Nkosazana Dlamini-Zuma alisema Polisi watasambazwa maeneo mbalimbali barabarani kuhakikisha watu wanatii sheria bila shuruti na kuzingatia kanunu za kujikinga na corona.
Alisema ni marufuku wananchi kunywa pombe hadharani na kuzunguka nazo au kuhamisha kutoka eneo moja kwenda nyingine ikiwa ni njia ya kukabiliana na virusi vya corona.
Dlamini-Zuma amesema uamuzi wa kupiga marufuku pombe mwishoni mwa wiki ni kuzuia kuenea kwa virusi ambavyo vimesababisha wagonjwa wengi kulazwa hospitalini.