Wizara ya mambo ya nje ya Marekani imewaonya raia wa Marekani nchini Ethiopia kwamba haitaweza kuwahamisha iwapo hali ya usalama itazidi kuwa mbaya ghafla.
Afisa wa ngazi ya juu wa Marekani aliwataka raia wa Marekani kuondoka Ethiopia mara moja, akisema kuwa Washington haina mpango wa kuandaa uhamisho wa watu wengi, kama ilivyokuwa Afghanistan.
Marekani na Umoja wa Afrika zimekuwa zikiishinikiza serikali ya Ethiopia na waasi katika eneo la Tigray kumaliza mzozo wao, ambao umeua maelfu ya watu na wengine milioni mbili kuyahama makazi yao tangu ulipoanza mwaka mmoja uliopita.
Maafisa wa Marekani wanasema Marekani imesitisha kuidhinisha vikwazo dhidi ya pande zinazozozana, kwa sababu mazungumzo ya amani bado yanaendelea.