TAHARUKI imeibuka kwa wakazi wa West Pokot wakati wakiwa kwenye harakati za kuandaa mazishi ya jamaa yao mmoja aliyejulikana kwa jina la Kangrok Muriumeler ambaye amesemakana kuwa amefariki dunia.
Imeelezwa kwamba, Kangrok Muriumeler alitoweka nyumbani kwa wiki moja baada ya kusafiri kwenda jijini Nairobi. Baadaye ripoti ziliibuka kuwa ameuawa na mwili wake kupatikana katika Soko la Konglai ambapo ulikuwa umetupwa na kuanza kuoza.
Mwili huo ulichukuliwa na maafisa wa polisi na familia kupewa taarifa kuhusu kifo cha mpendwa wao. Baadhi ya jamaa wa Muriumeler walidai kuwa wamethibitisha mwili uliopatikana na wa ndugu yao.
Hivyo shughuli za maziko zilianza hapo hapo nyumbani kwao, lakini cha kushangaza wakati shughuli za mazishi zinaendelea jamaa alirejea nyumbani akiwa mzima wa afya, na kukuta wakazi wa eneo hilo wakiandaa mazishi yake jambo lililoibuka taharuki kubwa.
Wakazi walijua kuwa ndugu yao ameshafariki na walichokuwa wakishuhudia ilikuwa ni kama miujiza na wala si jamaa wao. "Nilikuwa na wakati mgumu kuwaelezea kuwa bado nipo hai. Walisema ilikuwa ni roho amewatembelea," alsiema.
Muriumeler alisema alikuwa amesafiri kwenda jijini Nairobi kuuza mifugo lakini hakufanikiwa kurejea nyumbani kama kawaida na hivyo kuanza kusakwa na familia. Visa vya familia kuwazika watu wasio wao hutokea mara nyingi haswa ambapo vipimo vya DNA vikiwa havijafanywa ili kuidhinisha kweli miili iliyopatikana.