Viongozi wa Afrika Magharibi wanatarajiwa kukutana kwa mkutano wa dharura siku ya Jumapili kujadili mapinduzi ya hivi majuzi nchini Niger.
Rais wa Nigeria Bola Tinubu anatarajiwa kuwa mwenyeji wa mkutano huo katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja.
Bw Tinubu kwa sasa ni mwenyekiti wa shirika la Kiuchumi la Kanda ya Afrika Magharibi, Ecowas.
Taarifa kutoka kwa rais ilisema alilaani mapinduzi hayo katika nchi jirani ya Niger na kuahidi kwamba "Ecowas na jumuiya ya kimataifa itafanya kila iwezalo kutetea demokrasia na kuhakikisha utawala wa kidemokrasia unaendelea kukita mizizi imara katika eneo hilo".