Mapigano Makali yanazidi kuendelea kati ya wanajeshi wa Sudan na wanamgambo wa RSF ambao kwa sasa wanafanya mapigano hayo katika kingo za Mto Nile, tangu mapambano hayo yaanze sasa ni miezi minne.
Tovuti ya DW imeripoti kuwa mashuhuda wa wamesema makombora na mizinga vimefyetuliwa kati ya jeshi lenye kambi upande wa magharibi mwa mto Nile na wapiganaji wa RSF waliopo ukingo wa mashariki mwa mto huo.
“Inaarifiwa mapambano hayo yamedumu kwa siku kadhaa sasa na baadhi ya makombora yameanguka katika makazi ya watu na kusabisha vifo,”imesema taarifa hiyo ya DW.
Mapambano baina ya pande hizo mbili yamezidi kuwa makali pia katika Jimbo la Darfur na wiki iliyopita wanamgambo wa RSF walidai kuchukua udhibiti wa sehemu kubwa ya jimbo hilo.
DW inaripoti kuwa juhudi za upatanishi bado zimegonga mwamba katika kuutafutia ufumbuzi mzozo huo ambao tayari umewauwa karibu watu 10,000 na kuwalazimisha mamilioni wengine kuihama nchi hiyo.