Abdoulaye Diop Waziri wa Mambo ya Nje wa Mali amesema kuwa zoezi la kuondoka wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa kaskazini mwa Mali litafanyika kwa wakati kama ilivyopangwa yaani ifikapo Desemba 31, licha ya wasiwasi wa Umoja wa Mataifa.
Umoja wa Mataifa kwa upande wake umesema kuwa unatiwa wasiwasi kwamba, kuondoka kwa wanajeshiwake kunaweza kutatizwa na kushtadi mapigano kaskazini mwa Mali ambako makundi hasimu yenye silaha yanafanya kila yawezalo kudhibiti eneo hilo.
Umoja wa Mataifa umesema kuwa, serikali ya kijeshi ya Mali bado haijaupatia kibali cha kutuma misafara yake ili kukusanya suhula na zana zao huko kaskazini mwa Mali. Kuondoka kwa kikosi cha wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa huko Mali (MINUSMA) kufikia mwishoni mwa mwaka huu wa 2023 ni sehemu ya kurekebisha upya mpango wa usalama ulioanzishwa na utawala wa kijeshi wa Mali uliochukua mamlaka mwaka 2020. Kikosi cha UN cha MINUSMA
Wakati huo huo wanamgambo wa kundi la Wagner na wanajeshi wa Mali wameanza kuwasili kaskazini mwa Mali ili kuchua nafasi ya kikosi cha MINUSMA kilichoamrishwa na utawala wa kijeshi wa Mali kuondoka nchini humo.