Agizo hilo limetolewa leo Ijumaa Februari 28, 2020 na Jaji James Makau wakati akitoa hukumu ya kesi tatu zilizofunguliwa dhidi ya Serikali ya Kenya.
Akitoa uamuzi huo, Jaji huyo wa Mahakama Kuu ameagiza safari hizo za ndege kutoka China kusitishwa kwa siku kumi.
Kesi hizo zilifunguliwa katika Mahakama Kuu na Chama cha Wanasheria Kenya, madaktari wawili na wakili mmoja dhidi ya waziri wa afya, waziri wa uchukuzi, Mamlaka ya Usafiri wa Anga na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Katika kesi hizo ya kwanza iliyofunguliwa na Chama cha Wanasheria Kenya ambapo chama hicho kiliomba mahakama kuzuia ndege kutoka China kuleta abiria nchini Kenya, ombi ambalo lilikubaliwa na Jaji Makau.
Katika kesi zote tatu walalamikaji walibainisha kuwa ndege ya China iliyowasili Kenya Jumatano Februari 26, 2020 ikiwa na abiria 239 kinyume na ushauri uliotolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO) wa kuzuia maambukizi ya virusi vya corona.
Habari zinazohusiana na hii
- Mgonjwa wa tatu wa corona Afrika aripotiwa Nigeria
- Corona yaingia New Zealand, vifo duniani vyafika watu 2,800
Jana Alhamisi Kenya ilisema itaendelea kupokea ndege za abiria kutoka China licha ya nchi hiyo ya barani Asia kukumbwa na maambukizi ya virusi vya corona.
Tayari nchi tatu barani Afrika zimesharipoti visa vya maambukizi ya virusi vya corona ikiwemo nchi ya Nigeria ambayo imeripoti kuwa na mgonjwa mmoja leo
Kabla ya kuripotiwa mgonjwa huyo nchini Nigeria, kulikuwa na kesi mbili za watu waliombukizwa corona katika bara la Afrika.
Kisa cha kwanza cha maambukizi ya corona kiliripotiwa nchini Misri ikifuatiwa na nchi ya Algeria.
Ugonjwa huo wa corona ambao umekuwa tishio ulianza nchini China mwaka jana mwezi Desemba na mpaka sasa ugonjwa huo umeenea kwenye zaidi ya nchi 40.
Mpaka sasa ugonjwa huo umesababisha vifo vya watu 2,857 huku kikiwa na maabukizi zaidi ya watu 83,000.