- Kesi zote za dharura ambazo zilipaswa kushughulikiwa katika mahakama ya Runyenjes zitapelekwa katika korti za Embu na Kerugoya
- Kaimu Jaji Mkuu Philomena Mwilu alisema majengo ya mahakama hiyo yatapulizwa dawa
Kaimu Jaji Mkuu Philomena Mwilu ameamuru kufungwa kwa mahakama ya Runyenjes kwa muda wa siku saba baada ya wafanyikazi wanane kuambukizwa COVID-19.
Mwilu, katika taarifa iliyotolewa Jumatano, Aprili 14 alisema wafanyikazi 8 kati ya 18 wa Mahakama katika korti wamepelekwa kujitenga kulingana na itifaki za Wizara ya Afya.
Maafisa wa Wizara ya Afya katika eneo hilo walitembelea mahakama hiyo Jumanne kutathmini hali hiyo na baada ya hapo walipendekeza kwamba majengo hayo yafungwe kwa muda.
Walipendekeza pia wafanyikazi wote kujitenga wakati wa kipindi hicho na vile vile kufanyiwa vipimo zaidi vya COVID-19 huku mahakama hiyo ikipulizwa dawa.
"Hatau ya kufungwa kutawawezesha wafanyikazi wote katika kituo hicho kupimwa Covid-19 na kujitenga kulingana na itifaki za Wizara ya Afya Covid-19, pia hatua hii itapelekea kudhibiti kwa kusambaa kwa maradhi hayo," Mwilu alisema.
Aliongeza kuwa kesi zote za dharura ambazo zilipaswa kushughulikiwa katika mahakama ya Runyenjes zitapelekwa katika korti za Embu na Kerugoya.
Haya yanajiri takriban wiki moja baada ya mahakama ya Karatina kufungwa kwa muda wa siku kumi baada ya mmoja wa wafanyakazi kunasa virusi vya corona.
Kwenye taarifa yake, Mwilu alisema mahakama hiyo itapulizwa dawa kwa muda ambao itakuwa imefungwa kabla ya shughuli za kawaida kurejelewa tena.
Wafanyakazi walioathirika walishauriwa kujitenga kulingana na itifaki za Wizara ya Afya.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.