Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Magazeti Septemba 7: Tuju aweka mali ya Ruto kwenye rada ya KRA

B915d750fc28d17c Magazeti Septemba 7: Tuju aweka mali ya Ruto kwenye rada ya KRA

Tue, 7 Sep 2021 Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke

Magazeti ya Jumanne, Septemba 7, yanatathmni hatua ya Chama cha Jubilee kumtaka Naibu Rais William Ruto kuweka wazi anavyolipa ushuru kufuatia kukiri kuwa 70% ya mali iliyoorodheshwa na Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i ni yake.

Magazeti haya pia yanaripotia kuwa aliyekuwa seneta mteule Paul Njoroge amewasilisha kesi ya kurefusha muhula wa Rais Uhuru Kenyatta na miezi mitatu.

1. Daily Nation Gazeti hili linaripotia kuhusu makombora yanayoendelea kutupiwa Ruto kutoka kwa wandani wa Uhuru kuhusu chanzo cha utajiri wake.

Mnamo Jumatatu, Septemba 6, wandani wa karibu wa Uhuru wakiongozwa na Katibu Mkuu wa Jubilee, Raphael Tuju na uongozi wa bunge la chama hicho walianzisha mashambulizi dhidi ya Ruto.

Walikosoa namna aliweza kupata mali hiyo yote kama ilivyofichuliwa na Matiang’i.

Tuju alisema kuwa kile kimesalia Ruto kufanya ni kutangaza wazi namna anavyolipa ushuru wake kwa Mamlaka ya Ukusanyaji wa Ushuru (KRA).

2. The Standard



Gazeti hili linaripoti kuwa aliyekuwa Seneta mteule Paul Njoroge Ben amewasilisha kesi katika Mahakama Kuu akitaka IEBC izuiwe kuandaa Uchaguzi Mkuu wa 2022 .

Njoroge anahoji kuwa kuandaa uchaguzi Agosti 9, 2022, itakiuka katiba.

Anadai kuwa muhula wa uongozi wa Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto unatakiwa kukamilika Novemba 28,2023 sababu waliapishwa kutwaa hatamu za uongozi Novemba 2017.

Mwenyekiti wa IEBC, Wafula Chebukati mnamo Agosti 8, 2021, alitangaza kuwa chaguzi za 2022 zitaandaliwa Agosti 9, 2022, na pia tenda ya kuchapisha kura na ununuzi wa vifaa vya dijitali zitakazotumika.

3. Taifa LeoHuku muda ukiendelea kuyoyoma kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2022, Taifa Leo linaripoti kuwa siasa chafu zimeanza tena kuenezwa.

Kulingana na gazeti hili, wanasiasa wanatumia nguvu kuwagawanya Wakenya kwa msingi wa kikabila huku wakirushiana matusi hadharani.

Akizungumza Jumapili, Agosti 5, katika Kanisa la Hardy P.A.G, Mbunge wa Makadara George Aladwa alieneza siasa za kikabila huku kiongozi wa Orange Democratic Movement (ODM) akikosa kumkanya.



Mbunge wa Kapseret Oscar Sudi, ambaye anakumbana na kesi kadhaa mahakamani kuhusu matamshi ya chuki alirekodi video fupi wiki jana akimtukana Matiang’i.

4. The Star The Star linaripoti kuwa kaunti zenye wafugaji wa kuhamahama huenda wakawa kwenye mstari wa mbele kupata chanjo ya COVID-19 ya Johnson and Johnson.

Hii ni moja ya hatua ya serikali kuhakikisha kuwa kufikia Disemba Wakenya milioni 10 wanachanjwa.

Kenya ni nyumbani kwa wafugaji wengi wa kuhamahama hususan katika maeneo yenye ukame kaskazini mwa nchini kama vile Isiolo na Marsabit.

Jamii zinazolengwa ni Turkana, Pokot, Samburu, Endorois, Tugen, Sabaot, Somali na Borana.

5. People DailyChapisho hili linaripoti kuwa serikali imepiga marufuku vizuizi vya polisi barabarani kote nchini.

Hii ni baada ya kuibuka kwa ripoti kuwa baadhi ya maafisa watundu wanatumia vizuizi hivyo kupokea mlungula.

Makao Makuu ya Idara ya Polisi (NPS) pia iliagiza malalamishi yote ya madereva yachunguzwe ili hatua mwafaka iweze kuchukuliwa dhidi ya maafisa hao wa trafiki.



Kufuatia mkutano wa Inspekta Jenerali wa Polisi, Hillary Mutyambai, Naibu Inspekta Jenerali Edward Mbugua na Kamanda wa Trafiki Mary Omari, ilibainika kuwa licha ya masharti mengine kuwekwa bado kuna ufisadi hususan miongoni mwa maafisa wa trafiki.
Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke