HATIMAYE madereva wa malori zaidi ya 200 kutoka Tanzania, Kenya na Uganda wamevuka kuelekea Sudan Kusini baada ya kukwama kwa siku nne kutokana na machafuko ya kisiasa nchini humo.
Katibu Mkuu wa Chama cha Malori Tanzania, Greyson Wimile alisema hayo jana wakati akizungumza na HabariLEO, Dar es Salaam.
Alisema baada ya madereva hao kukwama kwenye mpaka wa Sudan na Uganda, juzi malori hayo yalianza kuvuka mpaka baada ya viongozi wa kijeshi wa nchi hizo kuzungumza na kukubaliana kuwa magari yatakayovuka yatalindwa kutoka mpakani hadi mji mkuu wa nchi hiyo Juba.
Wimile alisema walikubaliana kuwa magari baada ya kushusha mizigo yatalindwa kutoka Juba hadi mpaka wa Uganda. Alisema viongozi wa madereva kutoka Tanzania wamepongeza hatua hiyo na kushauri ulinzi huo uwe wa kudumu.
“Madereva wengi wamekuwa wanapata matatizo lakini kwa hatua hii tunapongeza,” alisema Wimile na kueleza kuwa, malori mengi yaliyokwama yalikuwa yamebeba vyakula.