Maafisa wanne wa polisi wametiwa mbaroni nchini Kenya baada ya maafisa wa upelelezi kuvamia nyumba ambayo Waethiopia 37 walikuwa wakizuiliwa, yapata kilomita 16 kutoka mji mkuu, Nairobi.
Maafisa hao wanashukiwa kusaidia shughuli ya magendo ya binadamu na ulanguzi.
Waethiopia hao waliambia mamlaka ya Kenya kwamba walikuwa wakielekea Afrika Kusini kutafuta maisha bora, gazeti la kibinafsi la The Star liliripoti.
Msako unaendelea kumtafuta mwenye nyumba hiyo na washiriki wengine wa mtandao wa magendo.
Kenya ni njia ya kawaida ya kupita kwa wahamiaji wa Ethiopia wanaojaribu kuingia Afrika Kusini kinyume cha sheria, kulingana na shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM.
Shirika hilo linasema kuwa wahamiaji hao, ambao wengi wao ni wanaume kutoka mikoa ya Oromia ya Ethiopia na SNNP, wanaingia Kenya kupitia mpaka wa Moyale, kabla ya kuelekea Tanzania na hatimaye Afrika Kusini.