Jumuiya ya Madaktari Wasio na Mipaka (MSF) imesema kwa akali watoto 13 wanafariki dunia kila siku kutokana na utapiamlo wa kiwango cha juu katika kambi moja ya wakimbizi nchini Sudan.
Claire Nicolet, Mkuu wa Idara ya Dharura ya jumuiya hiyo nchini Sudan amesema mtoto mmoja anaaga dunia katika kila saa mbili katika kambi ya Zamzam kaskazini mwa mkoa wa Darfur, yenye wakimbizi 300,000.
Amesema, "Watoto ambao hawajapoteza maisha kutokana na utapiamlo mkali kambini hapo wapo katika hatari ya kufariki dunia katika kipindi cha kati ya wiki tatu na sita iwapo hawatatibiwa."
Katika hatua nyingine, Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa limeonya kuwa, bara Ulaya liwe tayari kubeba mzigo wa wakimbizi wa Kisudan, iwapo makubaliano ya usitishaji vita baina ya Jeshi la Sudan na Vikosi vya Msaada wa Haraka vya kijeshi (RSF), hayatasainiwa karibuni. Mapigano Sudan
Wakati huo huo, Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) linasema kuwa limepokea ripoti za watu wanaokufa kwa njaa nchini Sudan, na hivyo limezitaka wahusika katika mzozo unaoshuhdiwa nchini humo kuhakikisha kwamba misaada ya chakula inawafikia wanaohitajia.
Kwa mujibu wa shirika hilo la Umoja wa Mataifa, watu milioni 18 wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula nchini Sudan, mara mbili zaidi ya mwaka uliopita.
Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Masuala ya Kibinadamu imetangaza kuwa, zaidi ya watu 13,000 wameuawa na wengine 26,000 kujeruhiwa katika vita vinavyoendelea nchini Sudan tangu Aprili mwaka jana.