Rais wa Kenya William Ruto ametetea ziara zake nyingi nje ya nchi akisema zimenufaisha taifa hilo kiuchumi.
Bw Ruto amelaumiwa kwa kufanya idadi kubwa zaidi ya safari za nje kwa mwaka mmoja ikilinganishwa na watangulizi wake. Vyombo vya habari vya ndani vinasema amekuwa katika nchi 38 tangu aingie madarakani Septemba 2022.
Lakini katika hotuba yake Jumapili, Bw. Ruto alisema kupitia safari hizo, ameweza kupata ajira kwa Wakenya na kupata mikataba kadhaa ya nchi mbili iliyolenga kufungua soko la mazao ya Kenya.
"Kuna watu wanaohoji kwa nini ninafanya safari za nje. Hayo ni majukumu yangu kama rais. Mimi ndiye ajenti mkuu wa Kenya na balozi ambaye nitapanga jinsi nchi itasonga mbele,” Bw Ruto alisema akihudhuria misa moja kanisani.
Rais alisema alipata kazi 350,000 na fursa za uwekezaji kwa Wakenya wakati wa ziara za hivi majuzi nchini Saudi Arabia na Uchina.