Watoto wawili wameokolewa wakielea karibu na ufukwe wa ziwa Kivu siku chache baada ya mafuriko kuua zaidi ya watu 400 mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
"Ni muujiza, sote tulishangaa," kiongozi wa jumuiya ya eneo hilo Delphin Birimbi aliambia BBC. Wazazi wao wamefariki lakini jamii inawasiliana na watu wanaoweza kuwalea, Bw Birimbi anaongeza.
Haijabainika jinsi watoto hao wachanga walinusurika kwa karibu siku tatu katika ziwa hilo, lakini mashuhuda wanasema waliwaona wakielea kwenye vifusi.
Watoto hao waliokolewa Jumatatu - mmoja huko Bushushu na mwingine Nyamukubi, vijiji viwili vilivyoathiriwa zaidi na mafuriko yaliyotokea wiki jana, Bw Birimbi anasema.
Mkasa huo umesababisha hisia za kuhuzunisha katika vijiji hivyo vyenye mrundikano wa maiti zilizofunikwa kwa blanketi.