NYOTA mkongwe wa muziki wa dansi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Koffi Olomide ametuma salamu za rambirambi kwa Watanzania juu ya kifo cha Rais wa Awamu ya Tano, Dk John Magufuli.
Kupitia video fupi aliyojirekodi na kuiweka kwenye mitandao ya kijamii, msanii huyo amesema ameguswa na kifo cha kiongozi huyo hivyo anaungana na Watanzania kuomboleza.
Alisema Tanzania ni nyumbani kwake, hivyo kifo kilichotokea kimemgusa kwasababu aliyefariki ni kiongozi mkubwa.
“Mpendwa dada na kaka na Watanzania, Tanzania ni kama nyumbani kwangu najiona kama Mtanzania, nachukua nafasi hii kutuma salamu zangu za rambirambi kwasababu mmepoteza mtu mkubwa Rais Magufuli.”
“Ninahuzuni na ninaungana nanyi kuomboleza, nawapa pole familia yake, watoto, mke wake na Watanzania,” alisema.
Olomide ni miongoni mwa wasanii wa DRC wanaokubalika nchini na waliojizolea mashabiki wengi.
Mwezi uliopita alikuja kutumbuiza katika moja ya tamasha na kufanya kazi na wasanii wawili wakubwa wa hapa nchini, ambao ni Nassibu Abdul ‘Diamond Platinumz’ na Faustina Charles ‘Nandy’.