Kampeni za uchaguzi zinaendelea nchini Togo, kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa wabunge na wa kikanda Jumatatu ijayo nchini humo.
Ni kampeni ambazo zinafanyika baada ya mwishoni mwa juma lililopita, wabunge kuipigia kura katiba mpya yenye utata ambayo sasa italiondoa taifa kutoka utawala wa rais hadi wa bunge.
Rais Faure Gnassingbé ana siku kumi na tano kuitangaza rasmi, ambapo sasa rais atachaguliwa na wabunge na sio wananchi, hatua ambayo hata hivyo imekosolewa vikali na wapinzani nchini humo.
Hata hivyo licha ya maandalizi ya kura mbili kuendelea, tume ya uchaguzi huko Togo imelikataa ombi la kanisa Katoliki la kupeleka waangalizi na sasa imeendelea kukamilisha zoezi la kusafirisha vifaa vya kupigia kura.
Uchaguzi wa wabunge huko Togo utafanyika tarehe 29 mwezi huu wa Aprili mwaka huu, na baada ya kutangazwa rasmi kwa katiba mpya, bunge hili litakuwa na mamlaka ya kumchagua rais na sio tena wananchi.