Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kesho kuna matumaini zaidi kuliko jana

Mandela Zsc Kesho kuna matumaini zaidi kuliko jana

Thu, 21 Mar 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mwaka 1960, Serikali ya kikaburu ya Afrika Kusini ilifanya mauaji ya halaiki ya raia 69 wasio na hatia, huku wengine 180 wakijeruhiwa waliokua wanaandamana kupinga udhalimu wa serikali hiyo kwa watu weusi. Mauaji hayo maarufu zaidi kama ‘Sharpeville massacre’ yalitokea March 21 katika mji wa Sharpville, ambao leo unajulikana kama Gauteng.

Baada ya mauaji hayo chama cha ANC kiliamua kubadili mbinu ya mapambano, kwa sababu njia zote za kudai haki kwa amani zilifeli. Njia ya mazungumzo, maandamano na migomo hazikufaa tena katika kudai haki kwani Serikali ya kikaburu ilizuia watu wasiseme, wasifanye mikutano ya kisiasa, wala maandamano.

Hakukua na uhuru wa vyombo vya Habari wala uhuru wa maoni na yeyote aliyetoa maoni yasiyoifurahisha Serikali, aliishia gerezani ama kupotezwa. Walioandamana walipigwa risasi na kufa, kiufupi Serikali haikujali na hapo ndipo wakaanzisha harakati za ukombozi.

ANC wakaamua kubadili mbinu kwa kuunda kikundi cha kupigana msituni kiitwacho uMkhonto we Sizwe (MK), ambalo ni neno la kizulu lililomaanisha ‘Mkuki wa Taifa’ lakini haraka Serikali ya kikaburu ikatangaza kuwa kikundi hicho ni cha kigaidi na ikakipiga marufuku, Viongozi wa ANC wakakamatwa akiwemo Nelson Mandela na Walter Sisulu wakawekwa jela.

Ilikuwa ni usiku wa July 11, 1961 shambani kwa Muisrael mmoja aitwaye Arthur Goldreich huko Rivonia, yeye alikua akiwafadhili ANC kwa siri hivyo naye akajumuishwa na kuwekwa ndani pamoja na kina Mandela.

Baada ya kukamatwa Mandela aliwaambia wafuasi wake wasikate tamaa, waendelee na mapambano. Alitumia maneno ya kizulu ‘Ngethemba ngoba kusasa’ ambayo tafsiri yake kwa Kiswahili alimaanisha ‘kesho kuna matumaini zaidi kuliko juzi au jana na alihukumiwa kifungo cha kwa miaka 27 kutokana na harakati zake za kuupinga ubaguzi wa rangi, katika kisiwa cha Robben.

Hata hivyo, Kikundi cha MK kiliendeleza mapigano dhidi ya Serikali dhalimu ya makaburu. Mapigano hayo yalichukua muda mrefu sana. Wakati Mandela akisota gerezani, kikundi hicho chini ya uongozi wa Muzi Ngwenya kiliendeleza mapambano kikiweka ngome yake huko Swaziland mpaka kuja kufanikisha ukombozi hapo baadaye.

Baada ya kuachiliwa huru mwaka 1990, Mandela alianzisha sera ya maridhiano au sera ya amani baina yake na watu weupe nchini Afrika Kusini, jambo ambalo watu wengi hawakulitegemea, ambapo pia inaarifiwa waliokufa wakati wa maandamano wanakumbukwa kama sehemu ya siku ya haki za binadamu.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live