RAIS Uhuru Kenyatta ameungana na Rais wa Namibia, Hage Geingob na wengine barani Afrika, kuitaka jumuiya ya kimataifa kusaidia kuondolewa kwa vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Zimbabwe.
Katika hotuba zao kwa nyakati tofauti katika Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Rais Kenyatta na Rais Geingob walisema Umoja wa Mataifa ndio sehemu inapopatikana heshima baina ya nchi na nchi na muafaka kwa migogoro mbalimbali.
“Katika kipindi ambacho nchi mbalimbali duniani zinataabika kutokana na virusi vya corona, nchi kama Zimbabwe zimejikuta katika mateso makubwa yaliyosababishwa na vikwazo haramu vya kiuchumi,” alisema Rais Kenyatta katika hotuba yake iliyowasilishwa kwa njia ya video.
Alisema vikwazo hivyo vinampa wakati mgumu Rais wa Zimbabwe, Emerson Mnangagwa, katika juhudi zake za kuleta mabadiliko katika sera za kiuchumi nchini kwake.
“Wakati dunia ikihangaika kupambana na janga la covid- 19, baadhi ya wanachama wa Umoja wa Mataifa wanapata shida kupambana na janga hili kutokana na vikwazo vya kiuchumi vilivyowekwa na mataifa ya Magharibi,” alisema.
Katika kuunga mkono juhudi za kupambana na virusi vya corona nchini Zimbabwe, Rais Kenyatta alisema, kwa niaba ya wananchi wa Kenya, kwa mara nyingine anauomba Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa kusaidia kuondolewa kwa vikwazo vyote vya kiuchumi vilivyowekwa dhidi ya Zimbabwe na wananchi wake