Kenya inayokabiliwa na ukame imetoa msaada wa chakula kilichosafirishwa kwa ndege hadi nchi jirani ya Somalia.
Msaada huo umekumbwa na kizaazaa kwenye mitandao ya kijamii huku zaidi ya robo ya Wakenya wanaoishi katika maeneo kame wakikabiliwa na kiwango kikubwa cha uhaba wa chakula, kulingana na data za Umoja wa Mataifa.
Shehena hiyo ilijumuisha vyakula vya aina mbalimbali na dawa za aina mbalimbali, kwa mujibu wa taarifa ya jeshi la Kenya.
Ilisema msaada huo ulikuwa ukiwalenga waliokumbwa na milipuko ya wiki iliyopita katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu, ambayo ilisababisha vifo vya watu 120.
"Tunasikia uchungu ambao ndugu na dada zetu nchini Somalia wanapata na tunamshukuru Rais William Ruto kwa mpango huu ambao utasaidia kupunguza mateso ya majirani zetu," alisema Kanali Victor Kang'ethe.