Serikali ya Kenya inajiandaa kufanya punguzo la zaidi ya asilimia 33 katika ushuru wa umeme kuanzia mwezi Disemba 2021 ili kuweza kunusuru Shirika la umeme la taifa la Kenya Power lililo katika hatari ya kuanguka kiuchumi.
Punguzo hilo ni sehemu ya mapendekezo yaliyofikiwa na Kamati iliyoundwa na Rais Kenyatta ya kukagua gharama za manunuzi ya umeme ili kuweza kuongeza kasi ya uwekezaji wa kigeni pamoja na kukuza viwanda vya nchini humo.
Hatua hii inakuja wakati Shirika hilo la umeme lenye hisa asilimia 50.1 likiwa katika mtikisiko mkubwa wa uchumi uliochochewa na vitendo vya rushwa, kuongezeka kwa matumizi ya nishati ya jua katika viwanda pamoja na mfumuko mkubwa wa bei ya kununulia umeme.
Hata hivyo kulingana na uchunguzi wa Kiuchumi wa mwaka 2021, umebaini kuwa mwaka 2020 uzalishaji wa umeme ulipungua hadi kufika 11,603.6 GWh kutoka 11,620.7 GWh mwaka 2019, huku matumizi ya umeme wa majumbani yakiporomoka kutoka 8,854.0 GWh mwaka 2019 hadi 8,796.4 kwa mwaka 2020.