Wafanya maamuzi kuhusu mazingira wameanza kukutana hivi leo jijini Nairobi, Kenya, kujadili namna nchi zinaweza kufanya kazi pamoja kukabiliana na mizozo ya mazingira kama vile mabadiliko ya tabia nchi, uchafuzi wa mazingira na upotevu wa viumbe hai.
Mkutano huu ni wasita wa Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa, serikali, mashirika ya kiraia, wanasayansi na sekta ya kibinafsi.
Baadhi ya washiriki wamesema viongozi wamesahau kuwa raia hawaishi kwenye kisiwa na kwamba kuna uhusiano mkubwa kati ya uharibifu wa mazingira, mabadiliko ya tabia nchi na athari ambazo binadamu wanazishuhudia kwa sasa.
Katika mkutano huu, nchi wanachama zitajadili rasimu ya maazimio kuhusu masuala mbalimbali ambayo baraza hupitisha baada ya makubaliano na kisha nchi wanachama hutakiwa kuyatekeleza.
Katika duru ya mwisho ya mazungumzo yam waka 2022, yaliyofanyika Nairobi, serikali zilipitisha maazimio 14, ikiwemo kuunda chombo cha kisheria kupiga vita matumizi ya Plastiki, mkutano wa mwaka huu mataifa yakiwasilisha maazimio zaidi ya 20 yakiwemo namna bora ya kurejesha ardhi iliyoharibiwa, kukabiliana na dhoruba pamoja na kupunguza athari za kimazingira za uchimbaji wa madini ya chuma.
Hata hivyo wataalamu wameonya kuhusu nchi kuwa na vipaumbele tofauti, hali inayosababisha kushindwa kupata muafaka wa pamoja wa kidunia.