Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kenya: Mchungaji afunguliwa rasmi mashtaka kwa 'ugaidi'

Mahakama Yaamuru Mackenzie, Wengine 30 Kufanyiwa Uchunguzi Wa Kiakili Kenya: Mchungaji afunguliwa rasmi mashtaka kwa 'ugaidi'

Fri, 19 Jan 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mchungaji Paul Nthenge Mackenzie ameshtakiwa rasmi siku ya Alhamisi kwa makosa manne, likiwemo lile la "kuwezesha kutendeka kwa kitendo cha kigaidi", baada ya vifo vya wafuasi 429 wa dhehebu lake la kiinjilisti aliowahubiria kufunga hadi kifo nchini Kenya.

Aliyejiita mchungaji alikana mashtaka hayo alipofikishwa mbele ya mahakama katika mji wa kusini mashariki mwa Mombasa, miezi tisa baada ya kuzuiliwa kuhusiana na kisa hicho kilichotikisa nchi hii ya kidini katika Afrika Mashariki, amebainisha mwandishi wa shirka la habari la AFP.

Hati ya mashtaka inalenga jumla ya washtakiwa 95 na inataja makosa ya "kuwezesha kutendeka kwa kitendo cha kigaidi", "kumiliki kifungu kinachohusishwa na kosa dhidi ya sheria ya kuzuia ugaidi", "kushiriki katika shughuli za uhalifu zilizopangwa. ” na “itikadi kali za kidini”.

Dereva wa teksi kabla ya kujitangaza kuwa mchungaji, Paul Nthenge Mackenzie aliwekwa kizuizini kabla ya kesi yake kusikizwa mnamo Aprili 14, siku moja baada ya kupatikana kwa waathiriwa wa kwanza katika msitu wa Shakahola ambako “Kanisa lake la Kimataifa la Habari Njema” lilikuwa linakutana.

Utafiti uliofanywa katika eneo hili kubwa la "msitu" katika pwani ya Kenya tangu wakati huo umegundua miili 429 kwenye makaburi au makaburi ya halaiki.

Uchunguzi wa maiti ulifichua kwamba wengi wa waathiriwa walikufa kwa njaa, yumkini baada ya kufuata mahubiri ya Paul Nthenge Mackenzie ambaye alihubiri kufunga hadi kifo ili "kukutana na Yesu" kabla ya mwisho wa dunia mnamo mwezi wa Agosti 2023.

Baadhi ya waathiriwa, wakiwemo watoto, walinyongwa, kupigwa au kukosa hewa. Paul Nthenge Mackenzie anatarajiwa kukabiliwa na mashtaka mengine.

Siku ya Jumanne, waendesha mashtaka walitangaza kwamba wanataka kumshtaki kwa takriban makosa kumi yakiwemo, pamoja na manne yaliyotajwa Alhamisi, yale ya "mauaji", "kumlazimisha mtoto kuteswa" na "ukatili kwa mtoto".

Wakati wa kusikilizwa Jumatano juu ya mashtaka ya "mauaji", mahakama iliamuru kucheleweshwa kwa siku 14 kwa ajili ya kufanyika kwa uchunguzi wa kiakili kwa mchungaji na washtakiwa wenzake 30.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live