Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Katibu Mkuu mpya EAC ataja vipaumbele vyake

03f3f8f12651091c1f28070e229d48a7.jpeg Katibu Mkuu mpya EAC ataja vipaumbele vyake

Tue, 27 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

KATIBU Mkuu mpya wa Sekretaieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Dk Peter Mathuk ameanza kazi kwa kueleza vipaumbele vyake katika miaka mitano atakayohudumia jumuiya hiyo.

Miongoni mwa vipaumbele hivyo, amevitaja kuwa ni kupunguza gharama za mawasiliano katika ukanda huo, utekelezaji wa uhuru wa huduma na biashara, kufungua anga na kuoanisha viwango vya kodi baina ya nchi wanachama.

Vingine ni kukamilisha mchakato wa ukaguzi wa Ushuru wa Pamoja wa Nje ya EAC (CET) na maombi yake kuwa sawa katika ukanda huo.

Mathuki alitaja vipaumbele hivyo wakati wa hafla ya kumuaga Katibu Mkuu wa EAC anayemaliza muda wake, Balozi Liberat Mfumukeko iliyofanyika katika makao makuu ya jumuiya hiyo jijini Arusha, Tanzania.

Dk Mathuki alisema anakusudia kuifanya EAC kuwa eneo moja la kimtandao (ONA) kwa nchi zote wanachama na kupunguza gharama kubwa za mawasiliano katika ukanda huo.

Aliahidi kwenda mbali zaidi katika kuboresha uhusiano kwa kufanya kazi kwa kushirikiana na watunga sera na wafanyabiashara kupitia mipango ya mazungumzo ya sekta ya umma na binafsi.

"Nina amini mazingira mazuri ya sera ya biashara ya kikanda yanayozingatia mapendekezo kutoka kwa wafanyabiashara na sekta binafsi yatajenga ujasiri katika ukanda huu kuwa eneo la kuvutia uwekezaji na kitovu cha biashara," alisema.

"Ninahaidi kuwa ofisi yangu itakuwa wazi kila wakati kwa mashauriano, kujadili mawazona kupanga mikakati ya kutekeleza majukumu yetu vyema," alisema.

Alitoa mwito kwa wadau wote kushirikiana ili kufikia malengo ya EAC na watu wake kwa kujitolea kwa kiwango cha juu cha uadilifu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mfumukeko alisema katika uongozi wake kuanzia 2016 hadi 2021, EAC imepata mafanikio makubwa katika kutekeleza nguzo nne za mchakato wa mtangamano ambazo ni umoja wa forodha, soko la pamoja, umoja wa fedha na shirikisho la kisiasa.

Alisema mafanikio mengine yameonekana katika maeneo mbalimbali ikiwamo katika na kilimo, uvuvi, afya, elimu, maji na usafi wa mazingira, mifumo ya fedha na malipo, usafiri wa anga, sayansi na teknolojia, nishati, biashara na uwekezaji.

Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa EAC, Adan Mohamed alisema Balozi Mfumukeko ametoa mchango mkubwa kufanikisha mchakato wa mtangamano wa EAC katika miaka mitano iliyopita.

Chanzo: www.habarileo.co.tz