Kamanda wa kijeshi wa Sudan, Mohamed Hamdan Dagalo, anayejulikana kwa jina la Hemeti, ameunga mkono hatua ya Jenerali Abdel Fattah al-Burhan kuchukua madaraka.
Hemeti, ambaye alikuwa naibu kiongozi katika Baraza la Utawala lililovunjwa sasa, alisema Jenerali Burhan "alikuja kusahihisha mwenendo wa mapinduzi, na kulinda usalama na utulivu wa nchi".
Maandamano ya kupinga mapinduzi hayo yamekuwa yakiendelea, ingawa ushiriki wa Jumapili uliripotiwa kuwa mdogo kwa sababu ya kukatika kwa mtandao.
Maafisa wa usalama waliwarushia vitoa machozi waandamanaji na baadhi ya walimu waliokuwa wakiandamana walizuiliwa.
Waandamanaji wanataka kukomeshwa kwa utawala wa kijeshi baada ya Jenerali Burhan kuvunja utawala kiraia wa serikali.