Mkenya Joseph Irungu alias Jowie amehukumiwa kifo baada ya kupatikana na hatia ya kumuua mfanyabiashara Monica Kimani 2018.
Akitoa uamuzi huo Jaji wa mahakama kuu nchini Kenya Grace Nzioka alisema kwamba mauaji ya bi Monica Kimani yalifanywa kwa makusudi.
''Hakikuwa kitendo cha kujilinda, hakikuwa kitendo cha uchokozi, Kilipangwa kwa makusudi na kutekelezwa'', aliamuru Jaji Nzioka.
Akitoa uamuzi huo jaji huyo aliangazia malalamishi ya upande wa mashtaka kuhusu madhara makubwa na mabaya yaliyotokea kwa marehemu" kwa kutumia silaha waliyoelezea kuwa "hatari."
Aidha alibainisha mpango wa mauaji hayo , na kuongeza kuwa hakukuwa na kiwango cha uchochezi kutoka kwa marehemu kwa mshtakiwa.
Mwezi uliopita Jowie alipatikana na hatia ya mauaji ya Monica Kimani, aliyeuawa kikatili katika nyumba yake ya Lamuria Gardens jijini Nairobi usiku wa Septemba 19, 2018.