Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Je Kenya iko tayari kwa uchaguzi mkuu?

Viongozi Kenya Je Kenya iko tayari kwa uchaguzi mkuu?

Fri, 31 Dec 2021 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Uchaguzi mkuu wa Kenya unaotarajiwa mwezi Agosti 2022, utakuwa ukurasa wa kupisha uongozi mpya utakaochukua usukani kutoka kwa utawala wa Rais Uhuru Kenyatta ambaye ameiongoza Kenya tangu mwaka 2013 kwa kipindi cha mihula miwili madarakani kupitia chama cha Jubilee.

Viongozi kadhaa wameonesha nia ya kutaka kuwania urais akiwemo naibu wa rais William Ruto ambaye anatarajiwa kuwania wadhifa huo sio kupitia chama kilichomuingiza madarakani cha Jubilee bali chama kipya cha United Democratic Alliance UDA kinachonadi sera zake kama chama kinachojali maslahi ya Wakenya wa tabaka la chini,wanaohangaika kila siku kusaka tonge ili angalau wapeleke mkono kinywani.

'Wahusika wakuu'

Bwana Ruto aneyejiita 'Hustler' ni naibu rais wa Kenya tangu mwaka 2013 mpaka sasa katika serikali ya Rais Uhuru Kenyatta chini ya chama tawala cha Jubilee.

Uhusiano kati yake na Rais umedorora na umezidi kuwa mbaya kila uchao, chanzo cha mkwaruzano huo hakijulikani wazi lakini inakumbukwa maji yalianza kuzidi unga punde baada ya Rais Uhuru Kenyatta kuafikia makubaliano ya kuleta maridhiano ya kitaifa na kiongozi wa upinzani Raila Odinga lengo likiwa kutuliza uhasama wa kisiasa nchini.

Mwingine anayetafuta kuliongoza taifa la Kenya ni kiongozi huyo wa muda mrefu wa upinzani Raila Odinga wa chama cha Orange Democratioc Movement ODM ambaye hivi karibuni amezindua rasmi azma yake ya kuwania urais kwa mara ya tano.

Katika miaka ya hivi karibuni, Bwana Raila Odinga almaarufu 'Baba' kama anavyoitwa na wafuasi wake, amekuwa na uhusiano wa karibu kisiasa na Rais Uhuru Kenyatta ambaye zaidi ya mara moja amedokeza hadharani ni upande gani kisiasa anaegemea kati ya Raila Odinga na naibu wake William Ruto bila ya kutaja jina la yeyote.

Mshirika wa Bwana Odinga kisiasa katika uchaguzi uliopita Musalia Mudavadi wa chama cha Amani National Congress ANC pia ashadokeza mapema nia ya kuwa rais wa tano wa Kenya katika uchaguzi huo wa Agosti 2022.

Si hao tu kuna gavana wa Makueni Profesa Kivutha Kibwana, Makamu wa rais wa zamani Kalonzo Musyoka, mwimbaji wa miziki ya injili Reuben Kigame miongoni mwa wengine wengi.

Hiyo ni katika ngazi ya urais, lakini uchaguzi huo utakuwa pia wa kuchagua viongozi wa nyadhifa nyingine ambazo ni Ugavana wa kaunti zote 47, maseneta, wabunge,wawakilishi wa wanawake na wawakilishi wa wodi.

Lakini huku macho yakielekezwa kwa uchaguzi huo, maswali ni mengi hasa kuhusiana na maandalizi na mazingira ya kuandaliwa kwake.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live