RAIS wa zamani wa Afrika Kusini, Jacob Zuma ameuomba umma kumchangia fedha zitakazomwezesha kukabiliana na kesi inayomkabili kuhusu tuhuma za rushwa.
Katika ukurasa rasmi wa twitter wa taasisi yake, amewataka raia wa Afrika Kusini kumshika mkono kwa kumchangia fedha zitakazomsaidia kulipia gharama za wakili.
Ujumbe huo umeambatana na namba ya akaunti ikiwa na jina la ‘JG Zuma.’
Zuma anatumikia kifungo cha miezi 15 tangu aliposhtakiwa kwa kuidharau Mahakama kwa kushindwa kufika mahakamani kusikiliza kesi dhidi yake kuhusu tuhuma hizo za rushwa.
Mapema mwezi huu, Zuma alikuwa amelazwa hospitalini hivyo kuchelewesha kuanza kusikilizwa kwa kesi yake dhidi ya tuhuma za rushwa.
Anakabiliwa na kesi mbili ikiwa ni pamoja na ufisadi na ulaghai.
Mwenyewe amekanusha tuhuma zote dhidi yake na kudai kuwa kesi hiyo ina ushawishi wa kisiasa.