Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

ICC yasitisha uchunguzi wote wa uhalifu uchaguzi wa Kenya

ICC Yasitisha Uchunguzi Wote Wa Uhalifu Uchaguzi Wa Kenya ICC yasitisha uchunguzi wote wa uhalifu uchaguzi wa Kenya

Wed, 29 Nov 2023 Chanzo: Voa

Mwendesha mashtaka mwandamizi wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu Jumatatu alitangaza kuwa anasitisha uchunguzi wote kuhusu uhalifu uliotendwa nchini Kenya ambapo unahusishwa na ghasia zilizozuka kufuatia uchaguzi wa mwaka 2007.

Uamuzi huo uliofikiwa na naibu mwendesha mashtaka mkuu wa ICC Nazhat Shameen Khan unamaliza mivutano ya kisheria ya miaka 13 iliyohusisha wanasiasa wa ngazi ya juu wa Kenya.

Mnamo mwaka 2010, mahakama yenye makao yake The Hague ilianza kuchunguza ghasia za uchaguzi katika taifa la Afrika Mashariki ambapo waendesha mashtaka walisema watu 1,300 walifariki na wengine karibu 600,000 waliachwa bila ya makazi.

Hapo awali, washukiwa sita walikabiliwa na mashtaka ya uhalifu mbalimbali dhidi ya ubinadamu, ikiwemo mauaji na kufukuzwa nchini.

Washukiwa hao ni pamoja na aliyekuwa rais wa zamani na wa sasa Uhuru Kenyatta na William Ruto mtawalia.

Lakini mwendesha mashtaka mkuu wa zamani Fatou Bensouda alifuta mashtaka dhidi ya Kenyatta mwaka 2014 na 2016 kusitisha kesi dhidi ya Ruto pia, baada ya majaji kusema ushahidi wa upande wa waendesha mashtaka ulikuwa dhaifu sana.

Kesi dhidi ya wote sita iligonga ukuta kutokana na kukosekana ushahidi.

Bensouda alilaumu juhudi nzito za kampeni za kuwatishia waathirika na mashahidi ili kuifanya kesi hiyo kuwa ngumu na waendesha mashtaka walianzisha uchunguzi mpya kuhusu vitisho dhidi ya mashahidi na rushwa.

Mwendesha mshtaka wa sasa Karim Khan alikuwa wakili wa Ruto wakati huo na alijitoa katika uchunguzi huo wa Kenya baada ya kuchukua nafasi ya Bensouda mwaka 2021.

Wakili wa Kenya Paul Gicheru alijisalimisha yeye mwenyewe katika mahakama ya ICC mwishoni mwa mwaka 2020, lakini kesi ya ushahidi ya rushwa dhidi yake ilitupiliwa mbali mwaka jana baada ya habari za kifo chake.

Washukiwa wengine wawili katika kesi ya rushwa na vitisho, Philip Bett na Walter Barasa bado hawajapatikana na wanakabiliwa na mshataka kadhaa katika mahakama hiyo.

Lakini naibu mwendesha mashtaka Nazhat Shameen Khan Jumatatu alisema anafunga uchunguzi zaidi kuendelea kuhusiana na ghasia za baada ya uchaguzi nchini Kenya.

“Nimefikia uamuzi huu baada ya kutafakari ukweli husika na mazingira ya hali hiyo,” alisema katika taarifa yake.

“Kama ilivyo, ofisi hiyo haitafuatilia kesi za ziada kuhusiana na madai ya uwajibikaji wa kiuhalifu wa watu wengine,” Khan alisema.

Chanzo: Voa