Serikali ya kijeshi nchini Niger imebatilisha karibu pasi za kusafiria za kidiplomasia elfu moja ambazo rais aliyepinduliwa Mohamed Bazoum alikuwa ametoa na kuwapatia maafisa na raia wa kigeni aliokuwa na uhusiano nao wa karibu.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Niger, imetoa tangazo kupitia barua ambayo imesambaa kwenye mitandao ya kijamii, ikiziarifu balozi zake za kidiplomasia nje ya nchi juu ya kubatilishwa kwa pasipoti hizo.
Barua hiyo inaeleza kuwa zaidi ya paspoti 990 za kidiplomasia za waliokuwa wakuu wa taasisi, mawaziri, wabunge, washauri na wasaidizi maalumu wa zamani katika ofisi ya rais, bunge na baraza la mawaziri zimebatilishwa.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, paspoti zipatazo 50 kati ya hizo zilitolewa kwa raia wa kigeni ikiwa ni pamoja na wa nchi za Ufaransa, Uingereza, Libya, Marekani, Uturuki na wa mataifa mengine ya Afrika Magharibi.
Hapo awali, serikali ya kijeshi ya Niger ilibatilisha pasi za kusafiria za kidiplomasia za maafisa watano wa serikali iliyopinduliwa ambao walikuwa nje ya nchi.
Mnamo Julai 26, vikosi vya walinzi wa rais wa Niger vilimuondoa madarakani rais Mohamed Bazoum kwa tuhuma za ufisadi, kushirikiana na nchi za Magharibi na kutojali umasikini walionao raia wa nchi hiyo. Jeshi la Niger limetupilia mbali miito ya Umoja wa Mataifa, nchi za Magharibi na ECOWAS ya kulitaka limrejeshe Bazoum madarakani.../