JANA timu ya Express ya Uganda imetangazwa kuwa mabingwa wapya wa kombe la Kagame baada ya kuifunga Nyasa Big Bullets ya Malawi bao 1-0 kwenye mchezo wa fainali uliopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Katika mashindano hayo yaliyofanyika jijini Dar es Salaam Tanzania kwa msimu huu yalihusisha jumla ya timu nane za Express, Nyasa Big Bullets, KMKM, Azam, Yanga, Atlabara, Le Messager Ngozi na KCCA zote kutoka ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Sambamba na Express kubeba ubingwa huo, nafasi ya pili imekamatwana Big Bullets huku KMKM ya Zanzibar ikimaliza katika nafasi ya tatu baada ya kichapa Azam bao 1-0 kwenye mechi ya kuwania nafasi hiyo.
Beki wa Big Bullets Yamikani Fodya ndiye aliibuka mchezaji bora wa mashindano hayo, kipa wa Express, Joel Mutakubwa akiibuka kipa bora, na Erick Kambale, Mutyaba Muzamiru wa Express na Paul Peter wa Azam wakiwa wafungaji bora kwa kufunga bao tatu kila mmoja huku nahodha wa Big Bullets Chimwemwe Idana kuchukua tuzo ya mchezaji muungwana.
Hii ni kwa mara ya kwanza kwa Express kubeba ubingwa huo baada huo, huku Simba ambayo haijashiriki msimu huu ikiongoza kwa kuwa bingwa mara nyingi zaidi ikiwa imebeba mara sita ikifatiwa na Tusker, Gor Mahia na AFC Leopards za Kenya pamoja na Yanga zilizobeba mara tano kila moja.