Addis Ababa. Ethiopia haitashiriki awamu ya mwisho ya mazungumzo kati yake na Misri na Sudan ambayo yanatarajiwa kufanyika wiki hii kuhusu mzozo juu ya mradi wa ujenzi wa bwawa la umeme katika Mto Nile.
Kwa mujibu wa shirika la habari la DW, Wizara ya Maji ya Ethiopia imethibitisha kutoshiriki mazungumzo hayo ambayo yanasimamiwa na Marekani.
Makubaliano ya mwisho kuhusu mradi wa bwawa kubwa la umeme yalitarajiwa kufikiwa mwezi huu lakini Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Mike Pompeo alisema kwenye ziara yake wiki iliyopita nchini Ethiopia kwamba makubaliano hayo sasa yanaweza kuchukua miezi kadhaa kwa kuwa bado kuna kazi kubwa ya kufanywa.
Ethiopia haitashiriki mazungumzo hayo yaliyopangwa kufanyika leo Februari 27 na kesho mjini Washington DC kwa sababu ujumbe wa nchi hiyo haujahitimisha uchunguzi wake na wadau muhimu, hii ikiwa kwa mujibu wa wizara hiyo ya maji, umwagiliaji na nishati.
Wizara hiyo imesema tayari wamemuarifu Waziri wa Fedha wa Marekani kuhusiana na hatua hiyo. Wakati Ethiopia ikisusia mkutano huo, tayari ujumbe wa Sudan umewasili nchini Marekani kwa ajili ya mazungumzo hayo.