Baada ya Marekani na Ufaransa, sasa ni zamu ya Umoja wa Ulaya kushutumu uungaji mkono wa Rwanda kwa kundi la waasi la M23 ambalo linaendesha harakati zake mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari, jumatatu ya wiki huu EU ilisema ina wasiwasi mkubwa na kuongezeka kwa ghasia katika eneo hilo na hali mbaya ya kibinadamu.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Umoja wa Ulaya umeeleza kuguswa na ongezeko la mapigano kati ya jeshi la serikali FARDC na waasi wa M23 Mkowani Kivu kaskazini, hali ambayo imesababisha maelfu ya raia kukimbia makazi yao.
Aidha EU imeoneshwa kusikitishwa kuona waasi hao wanatumia makombora ya kudungua ndege, ambayo hivi karibuni UN ilitaja wanapewa na nchi ya Rwanda, umoja huo ukilaani mashambulio ya hivi karibuni kwenye mji wa Sake na Goma.
Tamko hili linakuja wiki mbili baada ya Marekani na Ufaransa kuitaka Rwanda kuacha usaidizi wake kwa waasi hao, zikitoa wito wa majadiliano kutafuta suluhu ya kudumu.