Viongozi wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za Afrika Magharibi, ECOWAS wamekubaliana kutuma wanajeshi nchini Guinea Bissau kulisaidia taifa hilo kurejesha uthabiti kufuatia jaribio la mapinduzi lililoshindwa mapema wiki hii
Uamuzi huo umefikiwa wakati wa mkutano wa viongozi wa kanda ya ECOWAS yenye wanachama 15 uliofanyika jana mjini Accra nchini Ghana. Hata hivyo taarifa iliyotolewa haikueleza kwa undani hasa ni lini na hata idadi ya wanajeshi watakaopelekwa Guinea Bissau.
ECOWAS ilikwishawahi kutuma ujumbe kama huo wa kijeshi nchini Guinea Bissau kuanzia mwaka 2012 hadi 2020 baada ya kutokea mapinduzi ya kijeshi.
Dhima yake ilikuwa ni kuwazuia wanajeshi kuingilia siasa za nchi hiyo na kuwalinda viongozi wa kisiasa.
Uamuzi huo wa ECOWAS yumkini umechochewa na taarifa ya serikali ya Guinea Bissau iliyosema jaribio la mapinduzi la siku ya Jumanne wiki hii lilipangwa kwa ustadi mkubwa na inaonesha lilifadhiliwa vizuri.