Safari ya miaka 16 ya David Nyawade kutoka nchini Kenya aliyohudumu kama daktari imefikia tamati baada ya Baraza la Madaktari na Madaktari wa Meno nchini humo (KMPDC) kutoa taarifa kuwa hakuwa na taaluma hiyo na kuifungia leseni yake.
“Wagonjwa wanashauriwa kutopata huduma za David Nyawade Onyango,”ilisema sehemu ya taarifa ya KMPDC.
Daktari huyo anayetajwa kuwa ‘feki’ katika wasifu wake inaonyesha kuwa alisoma Chuo Kikuu cha Makerere kwa masomo yake ya shahada ya kwanza na baadaye alisoma katika Chuo Kikuu cha Stanford mnamo 2020, akibobea katika upasuaji wa mishipa.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa KMPDC, Dkt David Kariuki, amesema baada ya uchunguzi wa kina waligundua kuwa baadhi ya nyaraka alizokuwa nazo Nyawade ni feki.
Nyawade anashtukiwa zikiwa zimepita siku kadhaa tangu mamlaka nchini humo zimshikilie Brian Mwenda, anayedaiwa kuwa wakili ‘feki’ ambaye kwa zaidi ya miaka kumi amekuwa akijitambalisha kama Wakili wa Mahakama Kuu ya Kenya huku akishinda kesi zote 26 alizozisimamia.