Viongozi wa majeshi kutoka nchi za Afrika Kusini, Tanzania, Malawi na Burundi, nchi ambazo zinaunda kikosi cha pamoja cha kulinda amani kilichoko chini ya Jumuiya ya SADC, SamiDRC, mwishoni mwa juma lililopita, wamekamilisha ziara yao mashariki mwa nchi ya DRC, ambapo walitoa hakikisho la kurejesha usalama kwa kushirikiana na vikosi vya Serikali, FARDC.
Wakuu hao wa majeshi kutoka Afrika Kusini, Malawi, Tanzania, DRC na Burundi, wametoa kauli hii hapo jana baada ya kukamilika kwa mkutano wao wa siku tatu mjini Goma Mashariki mwa DRC, kutathmini oparesheni ya pamoja inayoendeshwa chini ya jumuiya ya SADC
Kulingana na msemaji wa jeshi la FARDC Meja jenerali Sylvain Ekenge, mkutano huo ulilenga kutathmni oparesheni zinazoendeshwa kwenye uwanja wa mapambano pamoja na kuangazia mikakati kuimarisha oparesheni hizo.
Aidha majenerali hao wameahidi kuimarisha vikosi vya SADC vinavyoshirikiana na wanajeshi wa Burundi na jeshi la Congo FARDC katika mapambano dhidi ya M23.
Vikosi vya SADC vilitumwa mashariki mwa DRC Disemba mwaka jana kwa lengo la kuisadia serikali ya Kinshasa kurejesha amani na usalama mashariki mwa nchi hiyo.