Wakati zoezi la kupiga kura likiendelea nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) mamlaka za nchi hiyo zimesema kuwa mtandao hautazimwa wakati wote wa Uchaguzi kuanzia kupiga kura ambako zoezi lake linaendelea, kuhesabu hadi kutolewa kwa matokeo ya Uchaguzi huo
Hii inafuatia hofu ya mitandao ya kijamii kufungwa wakati huu huku kukiwa na hofu ya wizi wa kura
"Hapana, hatutazima mtandao kwa sababu hatuko katika hali ya vita au maasi ya wananchi" -Waziri wa Mambo ya Ndani Peter Kazadi amesema hayo wakati wa mkutano wake na Waandishi wa Habari muda mfupi baada ya yeye kutoka kupiga kura
Aidha ameonya kuwa wale wanaopanga kuvuruga mchakato wa uchaguzi watakamatwa, wakati huo huo mamlaka ya usafiri wa anga imetangaza kufunga mipaka ya nchi kavu na Baharini kwa saa 24 kuanzia leo kwa ajili ya zoezi la uchaguzi mkuu huo
Kulingana na Kurugenzi Kuu ya Uhamiaji, mipaka imefungwa kuanzia mapema Asubuhi ya leo, Jumatano Desemba 20.2023 hadi saa 11:59 Jioni kwa saa za ndani
Anga ya DRC imefungwa kwa safari za ndani ambazo hazijaidhinishwa, lakini safari za ndege za kimataifa zitaendelea kama kawaida
Zaidi ya wapiga kura milioni 40 wanastahili kupiga kura ili kumchagua Rais miongoni mwa wagombea 19, akiwemo Rais anayetetea kiti chake Felix Tshisekedi
Wapiga kura pia wanachagua wabunge na wawakilishi katika chaguzi za manispaa.